Pages

Wednesday 2 March 2016

Chelsea waitumbukiza Norwich hatarini


Norwich wamejipata eneo la hatari Ligi ya Premia baada ya kushindwa na Chelsea wakiwa kwao nyumbani Carrow Road.

Norwich walilazwa 2-1 kwenye mechi hiyo iliyochezwa Jumanne jioni, huku Chelsea wakiendelea kupanda kwenye jedwali chini ya meneja Guus Hiddink.

Beki wa Blues Kenedy alifunga bao kwa kombora alilochomoa akiwa hatua 20 kutoka kwa goli, baada ya sekunde 39 pekee kuchezwa.

Bao hilo ndilo la kasi zaidi kufungwa Ligi ya Premia msimu huu.

Diego Costa aliongeza la pili sekunde chache kabla ya mapumziko, ingawa alionekana kuotea.

Cameron Jerome aligonga mwamba wa goli kabla ya Nathan Redmond kufunga lakini bao lake halikutosha na Norwich walishindwa mechi yao ya nane katika mechi tisa.

Norwich wakishuka eneo la hatari, Chelsea wamepanga kwenye jedwali hadi nambari nane, mara yao ya kwanza kuwa sehemu ya juu ya jedwali tangu wiki ya kwanza ya msimu.

Wameenda mechi 12 ligini bila kushindwa.

Norwich watakutana na Swansea, walio alama tatu juu yao, Jumamosi nao Chelsea wakaribishe nyumbani Stoke siku nne kabla ya kucheza mechi ya marudiano hatua ya 16 bora katika Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya dhidi ya Paris St-Germain.

Matokeo ya mechi za EPL zilizochezwa Jumanne
  • Aston Villa 1-3 Everton
  • Bournemouth 2-0 Southampton
  • Leicester 2-2 West Brom
  • Norwich 1-2 Chelsea
  • Sunderland 2-2 Crystal Palace
BBC Swahili

0 comments:

Post a Comment

Want to comment? write down here