Pages

Thursday 24 March 2016

Bao la Samatta laibana Chad, Kenya yachapwa


Bao la Mshambulizi wa Taifa Stars lilitosha kuipa Tanzania ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Chad katika mechi ya kufuzu kwa kombe la mataifa ya Afrika.

Mkwaju wa Samatta kunako dakika ya 30 ya kipindi cha kwanza ilitosha kuipa Taifa Stars ushindi muhimu ugenini.

Kufuatia ushindi huo Taifa Stars ya Tanzania imeimarika na kutoshana nguvu na Nigeria inayoorodheshwa katika nafasi ya pili.

Chad nayo imetokomea ikiburuta mkia katika kundi hilo la G bila alama yeyote.

Nigeria hata hivyo imeratibiwa kuchuana dhidi ya vinara wa ligi hiyo Misri siku ya Ijumaa.
Katika kundi C, Benin ilisajili ushindi mkubwa wa amabao 2-1 ugenini dhidi ya wenyeji wao Sudan Kusini.

Mshambulizi wa klabu ya Uingereza ya West Brom Stephane Sessegnon, alifungua kivuno hicho kunako dakika ya 16 kabla ya kuhakikishia timu hiyo alama tatu muhimu zikiwa zimesalia robo saa mechi hiyo kukamilika.

Kufuatia ushindi huo Benin imejikita kileleni baada ya kuipiku Mali.

Mechi hiyo iliyochezewa Juba ilishuhudiwa na rais mpya wa FIFA Gianni Infantino.

Kenya kwa upande wake itajilaumu yenyewe baada ya kupoteza nafasi nzuri ya kuipiku Guinea nyumbani kwao iliposhindwa bao moja kwa nunge Ugenini.

Harambee Stars ya Kenya ambayo imebadilisha kocha, ilifika Guinea na wachezaji wa nyumbani kabla ya kujiunga na wachezaji wake wa kigeni siku ya mechi.

Kufuatia kichapo hicho Kenya ndio inayoburuta mkia katika kundi hilo bila ushindi wowote.
Vinara wa kundi hilo Zambia na Congo walitoka sare ya bao 1-1.

Katika mechi nyingine Sao Tome na Principe ilitoka nyuma na kuilaza Libya 2-1 katika kundi F.

BBC Swahili

0 comments:

Post a Comment

Want to comment? write down here