Pages

Wednesday 6 April 2016

Yanga: Kambi Pemba itatoa majibu Jumamosi


UONGOZI wa klabu ya Yanga umeeleza kuwa kambi waliyoweka visiwani Pemba itawasaidia kuibuka na ushindi katika mchezo wa kwanza wa hatua ya 16 bora wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Al Ahly.

Yanga inatarajia kuvaana na Al Ahly, ambao ni vinara wa Ligi Kuu nchini Misri, katika mchezo utakaochezwa Jumamosi hii katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Kambi hiyo imeonekana kuwa na mafanikio kwa Yanga, ikumbukwe kambi hiyo ndio iliyomtia adabu Mnyama Simba kuangukia pua katika michezo ya Ligi Kuu Tanzania Bara katika mzunguko wa kwanza na wa pili.

Akizungumza na MTANZANIA jana, Ofisa Habari wa klabu hiyo, Jerry Muro, alisema matokeo hayo wanayoyatarajia, yatakuja baada ya Yanga kuwa na maandalizi mazuri Pemba kuelekea kwenye mechi dhidi ya Waarabu hao wa Misri.

“Tumeamua kwenda huko kwa kuwa ni sehemu tulivu na mara nyingi tumekuwa tukipata matokeo mazuri tukitokea huko, hivyo tunarajia kupata ushindi.

“Tulipata shida sana, lakini tuliweza kusafiri jana (juzi) na sasa tupo Pemba, wachezaji wataendelea na mazoezi yao kama kawaida tukijiandaa  na ushindi dhidi ya Al Ahly,” alisema Muro.

NA ADAM MKWEPU, MTANZANIA
Yanga ina ari ya kushinda mchezo wa kwanza hapa nyumbani, ili kujiwekea mazingira mazuri ikiwa ugenini.

0 comments:

Post a Comment

Want to comment? write down here